Mwaka huu una matukio makuu mawili ambayo yanasubiriwa kwa hamu kubwa na Watanzania wengi ili kuandika historia; upigaji kura wa kukubali au kuikataa Katiba Inayopendekezwa na Uchaguzi Mkuu wa Rais, wabunge na madiwani.Mambo hayo yanasababisha wanasiasa na vyama vyao kuwa katika hekaheka kubwa ili kuhakikisha wanashinda katika matukio hayo kulingana na msimamo wao.
Kumekuwapo na mgawanyiko katika suala la kuikubali au kuikataa katiba hiyo na mvutano mkubwa upo kati ya Serikali kwa maana chama tawala cha CCM na wapinzani chini ya muungano wao wa vyama vitatu, Chadema, CUF na NCCR-Mageuzi ambavyo vinaunda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa).
Silaha kubwa wanayoitumia Ukawa kwa sasa katika kuikabili CCM ni kashfa ya ufisadi ya Akaunti Tegeta Escrow na msimamo kwamba hawaiungi mkono Katiba Inayopendekezwa.
Kutokana na hali hiyo, CUF imefanya mkutano mkubwa wa hadhara kwenye uwanja wa Mashujaa mkoani Mtwara ambako ilitumia silaha hizo katika kushawishi wananchi kuiunga mkono.
Katika mkutano huo, mwenyekiti wa CUF, Profesa Ibrahim Lipumba alimwalika mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC), Zitto Kabwe ambaye kamati yake ndiyo ilishughulikia sakata hilo kwa kutumia taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG).
Ulikuwa ni mkutano uliopambwa na shangwe na nderemo za kila aina kutoka kwa wafuasi wa CUF waliojitokeza kuwalaki kwenye Daraja za Mikindani na kufanya maandamano ya zaidi ya magari 30, pikipiki 300 na bajaji 40 na pikipiki huku wananchi wakiwa wamejipanga kwenye mistari barabarani.
Baadhi walikuwa wakiimba nyimbo mbalimbali, zikiwemo zilizokuwa na kibwagizo cha “tunataka fedha zetu za Escrow zirudi... Mtumbwi wa Chenge umetoboka”. Andrew Change ndiye aliyekuwa mwenyekiti wa Kamati ya Uandishi ya Bunge Maalumu la Katiba.
Mbunge wa Mkanyageni, Habib Mnyaa (CUF) alitumia mkutano huo kuwaomba wananchi wa mkoa huo kupiga kura ya ‘hapana’ kwa Katiba Inayopendekezwa wakati muda utakapofika.
Alisema Chenge na wabunge wenzake wa CCM wametengeneza Katiba inayoendelea kulinda maslahi ya wachache badala ya Watanzania wote.
“Ikiletwa hapa katiba ya Chenge ikataeni. Ikataeni, tupeni kule kwani mkiikubali mtakuwa mnaungana na mafisadi kuhalalisha vitendo vya kifisadi viendelee.
“Fanyeni hivyo kwa maana maoni yenu yametupwa. Nanyi itupeni Katiba yao kwa kupiga kura ya hapana kwa wingi.
“Lakini hilo litaanza na ninyi kujitokeza kwa wingi kujiandikisha katika daftari la wapiga kura litakapoanza, bila hivyo hatutaweza kuipinga,” anasema Mnyaa.
Alisema: “CUF itakuwa nanyi bega kwa bega katika hili kwani tulitarajia kupata Katiba bora lakini imekuwa kinyume chake na hili halina ubishi kwani mlijionea ninyi wenyewe yaliyokuwa yanaendelea kuwa bungeni Dodoma.”
Profesa Lipumba aliwaomba wananchi waiunge mkono CUF kwenye Uchaguzi Mkuu wa Oktoba mwaka huu na akawashukuru kwa jinsi walivyokiunga mkono chama hicho kwenye Uchaguzi wa Serikali za Mitaa uliomalizika hivi karibuni.
“Wananchi wametuamini na kutuchagua sasa kazi ni kwetu kuwatumikia kwa weledi na kuonyesha tofauti yetu na walio kuwapo... Ongozeni kwa misingi ya chama kwa haki sawa kwa wote,” anasema.
Anaongeza: “Harakati za kuiondoa CCM madarakani imefika. Utakapofika wakati wa kujiandikisha katika daftari la kudumu la wapiga kura hakikisheni mnajitokeza kwa wingi ili muwe na fursa ya kuchagua na kuitupilia mbali CCM.”
Profesa Lipumba anasema, “Mabadiliko ya nchi hii yatafanywa na sisi wenyewe kama tutaamua. Dalili tayari mmeanza kuzionyesha mabadiliko kupitia Uchaguzi wa Serikali za Mitaa. Endeleeni hivyo hivyo kwani CCM imeshindwa na sasa haina uwezo tena wa kuendelea kutuongoza.”
Zitto na Escrow
Mwenyekiti wa PAC, Zitto Kabwe, ambaye ni mbunge kupitia Chadema, alieleza kwenye mkutano huo jinsi kamati yake ilivyofichua uozo katika sakata la escrow.
Anasema wizi wa fedha kwenye Akaunti ya Tegeta Escrow ulikuwa ni Sh306 bilioni na kusisitiza ni lazima zirejeshwe ingawa Rais Jakaya Kikwete wakati akiongea na wazee wa Mkoa wa Dar es Salaam Desemba 22 mwaka jana alisema siyo mali ya umma bali ni za IPTL.
“Serikali lazima ichukue hatua mara moja kuhakikisha fedha zilizokuwamo kwenye akaunti ya Tegeta Escrow Anarudi, uamuzi wa mahakama ya kimataifa unatekelezwa na fedha za umma zinarejeshwa Tanesco (Shirika la Umeme Tanzania) na zile za binafsi zinalipwa kwa wamiliki halali.